Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Ashatu Kijaji amesema Tanzania imefanikiwa kuzuia tani 216 sawa na asilimia 86 ya uzalishaji wa kemikali hatari kwa Tabaka la Ozoni ambazo zingeingia nchini na kuleta madhara.
Amesema mafanikio hayo yametokana na Tanzania kuungana na nchi nyingine duniani kuridhia na kusaini Itifaki ya Montreal mwaka 1987, ambayo imechangia katika hifadhi ya Tabaka la Ozoni.
Dkt. Kijaji amesema hayo wakati akizungumza katika Kipindi cha ‘Mazingira Yetu na Tanzania Ijayo’ kinachotayarishwa na Ofisi ya Makamu wa Rais na kurushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Septemba 16, 2024.
Amesema Itifaki hiyo pia imekuwa ni nyenzo muhimu katika kuchangia jitihada za kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi yanayochangia joto duniani.