"Sisi Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) ni wawezeshaji, tunawezesha watanzania kuweza kutekeleza miradi ya uwekezaji na leo hii tumebahatika kufika hapa katika mgodi unaitwa Matongo Gold Mine uliopo eneo la Nyamongo Wilaya ya Tarime Mkoa wa Mara",
"Mitambo hii mikubwa, mashine zinazoonekana, zinazotumika katika mchakato mzima wa uchenjuaji wa madini aina ya dhahabu hapa katika mgodi huu, vyote kwa pamoja vimewezeshwa kupitia TIC, ambapo wamepata msamaha wa ushuru wa forodha katika kuingiza mitambo na mashine ambazo zinaonekana"
Felix John ambaye ni Meneja wa Uhamasishaji Uwekezaji wa Ndani TIC, amesema hayo wakati maafisa wa kituo hicho walipotembelea mgodi wa dhahabu wa Matongo, uliopo Nyamongo, Tarime mkoani Mara ikiwa ni muendelezo wa kampeni ya kuhamasisha uwekezaji wa ndani inayoendelea Kanda ya Ziwa.