Baada ya pambano lao lililotarajiwa kufanyika Julai 20, mwaka huu kuota mbawa, hatimaye Mike 'Iron' Tyson na Jake Paul watapigana Novemba 15 mjini Texas nchini Marekani.
Watu 80, 000 wanaweza kuingia kwenye ukumbi wa AT&T kushuhudia pambano hilo la aina yake ambalo linahusisha mabondia hao wanaopishana miaka zaidi ya 20 kati ya Tyson na Jake ambaye anajinasibu kwa umri wake kumruhusu kumpiga Tyson lakini naye Tyson akitambia uzoefu wake.
Tyson ambaye mara ya mwisho kupanda ulingoni kupigana pambano la kulipwa ilikua mwaka 2005, alipanda ulingoni kwenye pambano kama hili mwaka 2020 alipopigana na Roy Jones na kutoka droo.
Hivyo, hili litakuwa la pili tangu aachane na mapigano ya kulipwa na amemtisha Jake kwamba atakutana na wakati mgumu sana kumkabili siku hiyo licha ya kukiri kwamba kasi yake ya sasa sio kama aliyotamba nayo miaka ya 1980.