Staa wa kufunga mipira ya mitupo mitatu 'Three Pointer' Jonas Mushi, amesema kwasasa hafikirii Ligi ya Mpira wa kikapu Mkoa wa Dar es Salaam (RBA).
Nyota huyo anayechezea timu ya JKT Stars ameliambia Mwanaspoti kuwa, kwa sasa mawazo yake yapo kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mchezo huo (BAL).
“Kama kupata zawadi ya ufungaji nimepata mara nyingi na si jambo geni kwangu kwenye RBA, kwa kweli nafikiria mashindano makubwa ya BAL niweze kuonekana. Sasa nafanya mazoezi binafsi ya gym kujiweka sawa kabla sijaingia viwanjani,” alisema Mushi
Amesema mipango ya mazoezi uwanjani amepanga kuanza mwishoni mwa mwezi huu Januari, katika Uwanja wa JKT na Kurasini.
“Kabla ya hapo nitawasiliana na kocha Phineas Kahabi, ambaye atanipangia ratiba atakayokuwa nayo ya mazoezi,”amesema Mushi
Amesema kocha huyo anayefundisha timu ya Unmatched Basketball, amekuwa akimpa mazoezi kabla ya kuanza msimu wa ligi ya RBA kila mwaka.