Burudani

Habari

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mashairi bado yanaishi

Mpoto Data Mashairi bado yanaishi

Thu, 21 Mar 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Ikiwa dunia inaadhimisha siku yake ya Kimataifa, Machi 21, 'Ushairi', baadhi ya wataalamu wa Fasihi wanaamini kuwa bado tanzu hiyo ina nafasi yake katika jamii.

Miaka ya nyuma, iliyokuwa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) , ambayo kwa sasa inajulikana kama TBC Radio, ilikuwa na kipindi maarufu cha 'Malenga Wetu'.

Kipindi hichi, cha takribani saa moja, kiliwaleta pamoja wataalamu wa mashairi kutoka Tanzania, wakichambua dhima za tungo mbali mbali na baadae kuzighani hewani kwa manufaa ya wasikilizaji.

Kikitiwa nakshi na Khalid Ponera na mwenzake Mohammed Ngombo, ambao pia, walikuwa ni wjauzi wa Ushairi, ama kwa hakika, kipindi hichi kilipata wafuatiliaji wengi sana, hasa ukizingatia kuwa kwa kipindi kile cha miaka ya 1980 kuelekea 1990, RTD ndio ilikuwa redio pekee kwa wakati huo.

Tanzu hii pia ilijizoelea umaarufu kwenye taasisi mbali mbali za elimu, kwani wanafunzi pia walifundishwa namna ya kutunga na kuandika mashairi, kwa kuzingatia vina na mizani, ambavyo vilikuwa ni vitu muhimu katika utunzi huo.

Washairi maarufu kama Sheikh Shaaban Robert, Profesa Mohamed Ilyas, Mohammed Seif Khatib na tungo kama Bahati haina Kwao, Titi la Mama Litamu na Chungu Tamu ni baadhi ya tanzu zilizopata umaarufu sana katika ukanda wa Afrika Mashariki, hasa kutokana na dhima zao na mchango wao katika kukuza lugha ya Kiswahili.

Mara kwa mara, yaliandaliwa matamasha makubwa ya Ushairi, yaliyowaleta pamoja manguli katika eneo hili, kwa lengo la kuburudisha na kuelemisha jamii.

Moja ya kumbi zilizoandaa matukio ya aina hii, ni ukumbi maarufu wa Nkrumah katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambapo wataalamu wa fasihi walikutana kusikiliza na kujadili dhima ya tanzu hii inayoakisi maisha ya binadamu.

Hata hivyo, pamoja na mabadiliko makubwa na ya kasi ya kiiteknolojia yanayoshuhudiwa ulimwenguni, baadhi ya wapenzi wa ushairi, bado wanaamini kuwa Tanzu hii ina nafasi yake katika maisha ya kila siku.

Nafasi ya Ushairi katika Jamii

Kulingana na Mgunga mwa Mnyenyelwa, msanii maarufu wa sanaa za majukwaani kutoka Tanzania, nyakati zote, kama ilivyokuwa huko nyuma, bado umuhimu wa ushairi uko palepale.

"Mashairi ya kijadi yalikuwa yanafuata mfumo wa vina na mizani, lakini tusisahau kuwa hata nyimbo za Bongo Fleva na nyinginezo bado ni ushairi unaofuata utaratibu wa tofauti, kwahiyo itoshe tu kusema kuwa Ushairi bado unaishi hadi leo hii," anaiambia TRT Afrika.

Mgunga, ambaye alipata umaarufu baada ya tungo yake ya Nenda Mwalimu, aliyoitoa baada ya kifo cha Baba wa Taifa la Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1999, anasisitiza kuwa Fasihi haipaswi kuwa kama maji kwenye mtungi, na hivyo ni vyema kubadilika kutokana na nyakati.

"Mashairi lazima yanyambulike, yaende kwenye kutongoa na kutamba, hatuwezi kuwa wafungwa wa jana kutokana na mabadiliko yanayoendelea sasa ulimwenguni," anasema.

Kulingana na Mgunga, Ushairi ni kama kazi ya Kimaabara ambayo inapaswa kuendana na kasi ya hadhira yake.

Wakati sehemu kubwa ya hadhira ikiwa imehamia kwenye mitandao ya kijamii, Mgunga anaamini kuwa wasanii wana kazi kubwa ya 'kupigania roho ya Ushairi', kuhakikisha kuwa inaendelea kukuza lugha na kuchokoza fikra.

Jitihada hafifu

Hata hivyo, pamoja na kuwa na majina maarufu katika nyanja ya Ushairi kama vile Profesa Mugyabuso Mulokozi, Kulikoyela Kahigi na Euphrase Kezilahabi ambao walikuwa ni manguli wa sanaa hiyo, Mgunga anaamini kuwa bado jitihada hazitoshi kuhakikisha kuwa Ushairi unaendelea kuishi.

"Wengi wanajitahidi kupokea vijti kutoka kwa manguli hao, lakini ukweli ni kwamba Ushairi bado una nafasi yake kwenye jamii," anaongeza.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live