Ubalozi wa Zambia nchini Tanzania, umethibitisha kukamatwa kwa malori 200 ya mizigo yaliyosajiliwa nchini Tanzania kwa tuhuma za kusafirisha mizigo bila kibali.
Taarifa iliyotolewa Ubalozini hapo inaeleza kuwa malori hayo yalikutwa yakiwa yamebeba magogo ya mti aina ya 'Mkula' bila kuwa na vibali maalumu.
Aidha ilieleza kuwa Serikali nchini Zambia, ilishapiga marufuku usafirishaji wa miti hiyo tangu mwaka 2016 kutokana na hatari ya kupotea kwa miti hiyo kufuatia uvunaji uliokithiri.
"Ni kweli tumezuia zaidi ya malori 200 ya mizigo ambayo yamesajiliwa kwa usajili wa Tanzania, kwasababu madereva hawakuwa na vibali maalumu vinavyowaruhusu kusafirisha miti hiyo na vinavyoonesha kuwa ni kweli miti hii imetoka katika nchi ya Congo" Imesema taarifa hiyo.
Mkula unatajwa kuwa mti unaotengeneza mbao zenye ushindani mkubwa katika soko la kimataifa, hali hii imepelekea Zambia kupiga marufuku usafirishaji holela wa miti hiyo na inaelezwa kuwa mwaka 2018 takribani malori 250 yalishikiliwa na mamlaka za nchini humo kwa kusafirisha miti hiyo bila kibali maalum.