Afrika

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Raila Odinga anavyoingia serikalini kwa ‘mlango wa nyuma’

Ruto X Odingaaaaaaaa Raila Odinga anavyoingia serikalini kwa ‘mlango wa nyuma’

Sat, 27 Jul 2024 Chanzo: Mwananchi

Ni 'mfalme' wa miungano ya vyama vya siasa na Serikali, ndivyo unaweza kumuelezea Raila Odinga, mwanasiasa mashuhuri katika siasa za Kenya, ambaye sasa yumo ndani ya Serikali ya Rais William Ruto.

Raila ni muasisi wa maridhiano maarufu 'handshake' ndani ya vyama vya siasa na Serikali, tangu wakati wa mfumo wa chama kimoja cha Kanu na sasa taifa hilo likiwa na mfumo wa vyama vingi.

Licha ya Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Ruto kusisitiza hakutakuwa na 'handshake' au Serikali ya 'nusu mkate' kama walivyoita wao, ujio wa maandamano ya Gen-Z umebadilisha msimamo wake na wa Serikali.

Amelazimika kuwaingiza wanachana wa Chama cha ODM cha Raila kwenye nafasi nyeti za uwaziri ndani ya Baraza la Mawaziri.

Ruto amelazimika kukubaliana na shinikizo la Gen-Z la kufanya mabadiliko kadhaa ikiwamo kuondoa Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2024 na kuvunja baraza la mawaziri.

Mara ya mwisho kuvunjwa baraza la mawaziri kulifanywa na Rais Mwai Kibaki, miaka 19 iliyopita.

Viashiria vya 'handshake' kati ya wawili hao vilianza baada ya Ruto kumpigia debe Raila anayewania nafasi ya Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AU) na uamuzi wa Raila kupinga hoja ya Gen-Z kutaka Ruto ajiuzulu.

Raila aliyezaliwa Januari 7, 1945 katika familia yenye ushawishi mkubwa kisiasa, baba yake, Jaramogi Oginga Odinga, alikuwa makamu wa rais wa kwanza wa Kenya na mtu mashuhuri katika harakati za kupigania uhuru.

Alikoanzia siasa

Maisha ya kisiasa ya Raila yalianza miaka ya 1980 alipoibuka kuwa mkosoaji wa utawala wa Rais wa wakati huo Daniel Arap Moi.

Uanaharakati na uongozi wake katika siasa za upinzani ulimfanya awe mwanasiasa mwenye nguvu na ushawishi kama ilivyokuwa kwa baba yake.

Umaarufu wake uliongezeka miaka ya 1990 alipounda Chama cha National Development Party (NDP) na alitetea demokrasia ya vyama vingi. Alihimiza mabadiliko ya Katiba ambayo ilipatikana mwaka 2010.

Mwanzo wa 'handshake'

Kupeana mikono au 'handshake' ni moja ya matukio ya historia ya kisiasa ya Raila katika kuridhiana kisiasa nchini Kenya.

Kwake tukio hilo ni juhudi za kuziba migawanyiko ya kisiasa na kuelekeza nchi kwenye utulivu na maendeleo, licha ya changamoto na mabishano ya kisiasa hasa kutokana na nchi hiyo kuwa na siasa za ukabila.

Kupeana mikono katika siasa za Kenya kuna umuhimu mkubwa wa ishara na utendaji, kila moja ikiashiria matukio muhimu katika historia ya nchi hiyo kuanzia kwa Moi, Kibaki, Uhuru Kenyatta na sasa Ruto.

Raila, Rais Moi

Wakati wa utawala wa Rais Moi mwishoni mwa miaka ya 1970 hadi mwanzoni mwa miaka ya 2000, Raila aliibuka kuwa kiongozi wa upinzani mwenye msimamo, akipinga utawala wa chama kimoja cha Moi chini ya Kanu.

Alichukua jukumu muhimu katika mageuzi ya kisiasa ya miaka ya 1990, akitetea demokrasia ya vyama vingi na hatimaye kuunda miungano iliyochangia kudhoofisha nguvu ya Moi kwenye mamlaka ya kiserikali na kisiasa.

Muungano wa Kisiasa

Baada ya Moi kustaafu uongozi wa nchi, Raila alijiunga na Muungano wa National Rainbow Coalition (NARC) wa Mwai Kibaki ulioshinda Uchaguzi Mkuu wa 2002.

Muungano huo uliashiria mabadiliko makubwa katika siasa za Kenya na kumaliza utawala wa muda mrefu wa Kanu.

Kutokana na uchaguzi wenye utata wa mwaka 2007 na ghasia zilizofuata, Raila alichukua jukumu muhimu katika maridhiano, ambayo yaliunda makubaliano ya kugawana mamlaka.

Raila alipewa nafasi ya Waziri Mkuu katika Serikali ya mseto na Rais Mwai Kibaki hadi mwaka 2013.

Baada ya uchaguzi wa 2013, Raila aliongoza Muungano wa Mageuzi na Demokrasia (CORD) ambao ulikuwa mpinzani dhidi ya Serikali ya Rais Uhuru Kenyatta. Muungano huu ulilenga kusukuma mageuzi ya uchaguzi na uwajibikaji zaidi wa kisiasa.

Uchaguzi mkuu wa 2017

Katika uchaguzi wa 2017, Raila alishindana na Uhuru Kenyatta kama kiongozi wa Muungano wa National Super Alliance (Nasa).

Alipinga matokeo ya uchaguzi kwa madai kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi, hali iliyosababisha mzozo wa muda mrefu wa kisiasa.

Kupeana mkono kati ya Raila na Kenyatta mwaka 2018 kulisababisha kubuniwa kwa Mpango wa Kujenga Umoja (BBI), uliolenga kuimarisha umoja wa kitaifa na kushughulikia masuala muhimu ya utawala kupitia mageuzi ya katiba.

Raila na Ruto

Katika Serikali ya sasa chini ya Rais Ruto, jukumu la Raila limebadilika akiendelea kuwa kinara katika siasa za Kenya, akitetea mageuzi na kushiriki michakato ya mazungumzo ya kitaifa.

Ushawishi wa Raila unachukua miongo kadhaa na unaonyesha kujitolea kwake kwa utawala wa kidemokrasia, mageuzi ya uchaguzi na umoja wa kitaifa nchini Kenya.

Uwezo wake wa kuunda miungano na kujadili suluhu za kisiasa umekuwa muhimu katika kuchangia hali ya kisiasa ya Kenya, ingawa juhudi hizo zimekuwa zikitambulika kwa ushirikiano na mizozo na tawala mbalimbali.

Mkono na Rais Kibaki

Kupeana mkono kati ya Raila na Kibaki mwaka 2008 labda ni mojawapo ya matukio ya kisiasa yenye matokeo katika historia ya Kenya.

Ilitokea baada ya uchaguzi wa Rais 2007 wenye utata, ambao ulikumbwa na madai ya wizi wa kura na ghasia zilizoenea ambazo ziligharimu maisha ya mamia ya watu.

Awali, Raila na wafuasi wake walipinga matokeo wakidai kulikuwa na udanganyifu katika uchaguzi.

Ghasia baada ya uchaguzi zilisababisha upatanishi wa kimataifa ulioongozwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, hayati Kofi Annan, ambao ulifikia kuundwa kwa Serikali ya mseto. Kupeana mkono kati ya wawili hao kulionyesha kujitolea kwa maridhiano na utulivu wa kitaifa.

Chini ya Serikali ya Muungano, Raila alishika wadhifa wa Waziri Mkuu, hivyo kuashiria makubaliano ya kihistoria ya kugawana mamlaka yenye lengo la kurejesha amani na kutekeleza mageuzi.

Serikali ya mseto ilisimamia mabadiliko makubwa ya kikatiba, ikiwa ni pamoja na kupitishwa kwa Katiba mpya mwaka 2010 ambayo ilitaka kugatua madaraka na kuimarisha usawa. Kupeana mkono kuliwakilisha kuondoa siasa za uhasama, kuwa na umoja wa kitaifa na maendeleo, badala ya masilahi ya vyama.

Kwa Raila ilikuwa ni hatua ya kimkakati kuhakikisha malalamiko ya wafuasi wake yanashughulikiwa, pia ilichangia kuimarisha demokrasia.

Muungano wa Azimio

Muungano wa Azimio la Umoja unaoongozwa na Raila ulishindwa kwenye uchaguzi uliopita na muungano wa UDA unaoongozwa na Ruto.

Muungano wa Azimio ulichukua nafasi muhimu katika uchaguzi wa Kenya wa 2022, na kuashiria sura muhimu katika nyanja ya kisiasa nchini humo.

Uliundwa kwa lengo la kuunganisha nguvu na uungwaji mkono ili kupata ushindi katika uchaguzi wa urais na ubunge.

Uliwaleta pamoja viongozi wakuu wa kisiasa na vyama, vikiwemo vya Wiper Democratic Movement cha Kalonzo Musyoka, Amani National Congress cha Musalia Mudavadi, na KANU cha Gideon Moi.

Kwa kutambua wapiga kura wa Kenya wenye makabila mbalimbali, Azimio la Umoja ilifanya kampeni kupunguza migawanyiko ya kikabila na kukuza uwiano wa kitaifa.

Muungano huo ulitumia sifa ya Raila kama kiongozi wa mageuzi aliyejitolea kushughulikia ufisadi na kuimarisha uwajibikaji katika utawala.

Changamoto

Muungano wa Azimio ulikumbana na changamoto kadhaa wakati wa kampeni za uchaguzi ukiwamo upinzani kutoka kwa miungano na vyama hasimu, hasa cha Ruto cha United Democratic Alliance (UDA).

Kampeni ya Ruto ilivutia sehemu kubwa ya wapigakura waliokatishwa tamaa na viongozi, akiahidi mtazamo mpya wa utawala na sera za kiuchumi.

Januari 2022, muungano wa Azimio la Umoja uliundwa kuunga mkono upande mmoja wa kisiasa, hasa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huo. Martha Karua, kupitia chama cha Narc Kenya alijiunga na muungano huo.

Mbali ya hilo, Januari 2022, muungano wa Ruto wa UDA unaojumuisha vyama kadhaa vya kisiasa uliundwa.

Vyama vikuu ndani ya UDA wakati huo vilikuwa ni United Democratic Alliance (UDA) cha Ruto alichoanzisha baada ya kuihama Jubilee.

Chama cha Maendeleo na Mageuzi (PDR) ambacho kiliunganishwa na UDA 2021, na kuongeza nguvu na ushawishi.

Pia, Chama cha Mashinani (CCM) kinachoongozwa na aliyekuwa Gavana wa Bomet, Isaac Ruto, People's Empowerment Party (PEP) kikiongozwa na Mbunge wa Gatundu Kusini, Moses Kuria na Service Party (S).

Chanzo: Mwananchi