Korea Kaskazini inatarajia kufunga Ubalozi wake uliopo nchini Uganda, hatua ambayo itahitimisha uwepo wake wa Kidiplomasia wa takribani nusu karne nchini humo.
Uamuzi huo ulitangazwa jana baada ya mkutano kati ya Rais wa Uganda Yoweri Museveni na Balozi wa Korea Kaskazini, Jong Tong Hak.
Balozi huyo alimueleza Museveni kuwa hatua hiyo ni katika kujaribu kupunguza idadi ya Balozi zao barani Afrika, ili kuongeza ufanisi wa taasisi za nje za nchi hiyo.
”Urafiki wetu mzuri utaendelea na utaimarishwa na kuendelezwa” alisema Balozi Hak
Korea Kaskazini ilianza uhusiano wa karibu na Uganda mwaka 1962 mara tu baada ya nchi hiyo kupata uhuru.
Pyongyang ilimuunga mkono Idi Amin alipoichukua nchi mwaka 1971 kwa kuyapatia majeshi yake mafunzo na silaha.
Mwaka mmoja baadaye nchi hiyo ilifungua ubalozi wake jijini Kampala.
Rais Yoweri Museveni amewahi kutembelea Korea Kaskazini mara kadhaa na kukutana na Kiongozi wa zamani wa nchi hiyo Hayati Kim Jong il ambaye ni baba wa Kiongozi wa sasa Kim Jong Un.