Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Museveni amemtetea mtoto wake kwa ujumbe wa siasa anaoandika Twitter

Museveni Amemtetea Mtoto Wake Kwa Ujumbe Wa Siasa Anaoandika Kwenye Twiter Museveni amemtetea mtoto wake kwa ujumbe wa siasa anaoandika Twitter

Tue, 20 Dec 2022 Chanzo: Voa

Rais wa Uganda Yoweri Museveni amesema kwamba haoni makosa yoyote kwa mwanawe kuzungumzia siasa za nchi hiyo licha ya kwamba sheria za nchi zinapiga marufuku wanajeshi kuzungumzia au kujihusisha na siasa.

Museveni ambaye amekuwa na msimamo mkali sana kwa makamanda wake wa jeshi kuhusiana na siasa kiasi cha baadhi yao kushitakiwa katika mahakama ya kijeshi kwa kuonyesha ishara za kujihusisha na siasa, amesema kwamba maafisa wa ngazi ya juu ya jeshi akiwemo mwanawe Muhoozi Kainerugaba hawataadhibiwa.

Generali Muhoozi Kainerugaba, mtoto pekee wa kiume wa rais wa Uganda Yoweri Museveni, amekuwa akiandika ujumbe wa kisiasa na mara nyingi wenye utata kwenye mtandao wa kijamii wa twiter.

Licha ya ibara ya 208 sehemu ya 2 ya katiba ya Uganda na ibara ya 3 sehemu ya (a) ya kanuni za jeshi la Uganda UPDF ya mwaka 2005 kupiga marufuku wanajeshi wote kujihusisha na siasa, Muhoozi ameandika sana kuhusu siasa za Uganda, kuwalenga wapinzani wa serikali ya babake, kutumia nafasi yake jeshini kuwaadhibu wanaokosoa serikali kama mwandishi wa mashairi Kakweza Rukirabashaija, kukosoa juhudi za kijeshi dhidi ya waasi wa M23 nchini DRC, kukosoa serikali ya Ethiopia katika vita dhidi ya wapiganaji wa Tigray TPLF, kutangaza kuunga mkono Russia kuvamia Ukraine, kutishia kuvamia Kenya kijeshi, miongoni mwa mengine.

Wanasiasa na wanaharakati nchini Uganda wamekuwa wakitaka Generali Muhoozi kuadhibiwa lakini Museveni katika mahojiano na gazeti la Uganda, amesema kwamba haoni shida magejerali wake wakizungumzia siasa.

Msimamo wa Museveni ni kinyume na hatua alizochukua dhidi ya magenerali wengine hasa Generali David Sejussa na Generali, Generali Henry Tumukunde, waliofunguliwa mashtaka ya uhaini katika mahakama ya kijeshi kwa kuzungumzia siasa za Uganda katika mahojino na waandishi wa habari.

Muhoozi, ameandika vile vile kwamba hana imani na chama kinachotawala cha National resistance movement NRM, kinachoongozwa na babake, akisema kwamba wanachama wake ni walafi na hawajali maslahi ya nchi.

Aliandika vile vile kwamba hakuna kitu kama demokrasia na kwamba la muhimu ni kufanya mapinduzi kwa kuzingatia maslahi ya watu.

Bila kutoa ufafanuzi zaidi, Generali Muhoozi Kainerugana aliandika kwamba waandishi wa habari ni magaidi na hata kutaja baadhi ya waandishi wa habari nchini Uganda akitishia kile alisema atawavunja vunja. Museveni, amesema hayo ni mambo madogo yasiyohitaji kumuadhibu mwanawe.

Tume ya kutetea hali za kibinadamu nchini Uganda, kwa sasa inachunguza visa vya watu kutoweka, ikiaminika kwamba wanakamatwa na maafisa wa usalama ambao hawavai sare za kazi wala kutumia magari ya kazi na yasiyokuwa na namba za usajili ambayo raia wa Uganda wanayaita kama drones.

Sababu ya ukamataji huo haijulikani lakini wanaokamatwa sana ni wapinzani wa serikali.

Chanzo: Voa