Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Hawa hapa mastaa 10 wa kutazamwa zaidi Olimpiki 2024

Mastaa 10 Hawa hapa mastaa 10 wa kutazamwa zaidi Olimpiki 2024

Wed, 24 Jul 2024 Chanzo: Mwanaspoti

Michezo ya Olimpiki ya Paris 2024 inatazamiwa kuanza Ijumaa hii huko Ufaransa kwa kushirikisha wachezaji 10,500 kutoka mataifa 206, Tanzania ikiwa ni miongoni mwao.

Katika mashindano hayo, kutakuwa na michezo 32 na Tanzania itashiriki katika michezo mitatu ya riadha, kuogelea na judo.

Garbriel Geay, Jackline Sakilu, Alphonce Simbu na Magdalena Shauri watashiriki marathoni, Collins Saliboko, Sophia Latiff kuogelea na Mlugu Thomas atachuana katika judo.

Katika michezo hiyo, Mwanaspoti linakuangazia baadhi ya mastaa wakubwa watakaoshiriki na wanatazamwa kuona watafanya nini katika kuwania medali.

ELIUD KIPCHOGE

Mkenya anayezungumzwa vyema kuhusu nafasi yake katika Michezo hiyo akilenga kushinda dhahabu ya tatu mfululizo katika kihistoria ya mbio za Olimpiki.

Mkimbiaji huyo wa marathoni mwenye umri wa miaka 39 licha ya umri mkubwa alionao, wengi bado wanaamini atafanya kitu mwaka huu na kuendelea kuweka rekodi.

"Bado nina kitu miguuni mwangu na nitakuwepo kugombea medali ya dhahabu," alisema Kipchoge.

Mwaka 2019, alikuwa binadamu wa kwanza kukimbia mbio za kilomita 42.2 (maili 26) chini ya saa mbili, ingawa rekodi hiyo haikuwa rasmi na muda haukuwekwa katika mashindano hayo ya wazi.

RAFAEL NATAL

Bingwa huyo mara 22 wa mchezo wa tenis huenda ikawa ndio mwaka wake wa mwisho wa maisha kwenye mchezo huo.

Mashindano ya tenisi ya Olimpiki ya Paris yatafanyika katika viwanja vya Roland Garros, Natal akiwa na rekodi ya kushinda mataji 14 hapo.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 38, ameshinda dhahabu mbili za Olimpiki, mwaka wa 2008 (singles) na 2016 (mara mbili pamoja na Marc Lopez).

Ni miongoni mwa nyota wanaotazamwa zaidi na mashabiki wa mchezo huo kuona mwisho wake utakuwaje.

LEBRON JAMES

Mfungaji bora wa muda wote wa NBA ndiye anayeiongoza timu ya mpira wa Kikapu ya Marekani na anatazamiwa kucheza mechi yake ya nne ya Olimpiki.

Nyota huyo mwenye umri wa miaka 39 atakuwa mchezaji wa kwanza wa mchezo huo kwa wanaume Marekani kushiriki Olimpiki tatu mfululizo.

SHELLY-ANN FRASER-PRYCE

Huyu ni malkia wa mbio fupi za viwanjani Jamaica na atashiriki Olimpiki yake ya tano na ya mwisho katika mbio za 100m za wanawake.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 37 ameshinda medali nane za Olimpiki, zikiwemo tatu za dhahabu.

Anajulikana kwa jina la utani 'Pocket Rocket', kutokana na kasi yake ya kuanza na kumaliza mbio na anatazamiwa pia kupata ushindani mkali kutoka kwa Mmarekani, Sha'Carri Richardson na Mjamaika mwenzake, Shericka Jackson.

Nyota hao watatu inaaminika wanaweza kuvunja rekodi ya miaka 36 ya Florence Griffith Joyner katika mbio za mita 100 za wanawake (10.49).

CAELEB DRESSEL

Caeleb Dressel alishinda medali tano za dhahabu huko Tokyo 2020 kisha akashtua ulimwengu wa kuogelea mnamo 2022 kwa kujiondoa ghafla kwenye mchezo ili kudumisha afya yake ya akili.

Katika kurejea kwake, mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 hajafuzu kutetea dhahabu yake ya mita 100, lakini alishinda mbio za mita 50 na butterfly 100, ikimaanisha atapata nafasi ya kutetea medali zake mbili za dhahabu katika Michezo ya Olimpiki ya Paris.

RAYSSA LEAL

Kijana wa Brazil anayevuma katika mchezo wa kuteleza kwenye barafu Rayssa Leal ataonekana kuvutia wengi kutokana na uchezaji wake wa hali ya juu.

Amepewa jina la utani 'mtu mdogo', anatazamiwa kufanya vizuri Paris kwa maana ya kupata medali ya dhahabu kwani ikumbukwe mwaka 2020 Tokyo alipata medali ya fedha.

Licha ya ubora wake na kupewa nafasi lakini itabidi afanye kweli na kumshinda Sky Brown wa Uingereza ambaye pia anatafuta kuboresha medali yake ya shaba kutoka Tokyo 2020, aliyoshinda akiwa na umri wa miaka 13.

VICTOR WEMBANYAMA

Mfaransa huyu ni mshindi wa tuzo ya mwaka wa Ligi Kuu ya Kikapu Marekani (NBA,) amejizolea umaarufu mkubwa katika mchezo huo kutokana na aina ya uchezaji wake.

Mwaka 2020 Tokyo, Ufaransa ilishindwa na Marekani katika mechi ya medali ya dhahabu na ndiye anayeongoza matumaini ya wengi kutwaa ubingwa na kuepuka yale ya Tokyo.

Nyota huyo mwenye urefu wa mita 2.24 (futi 7 na inchi 4), ndiye mchezaji mrefu zaidi katika michezo ya Paris 2024.

Wakati ufaransa ikipewa nafasi ya kutwaa medali ya dhahabu kutokana na urefu wa nyota huyo kwa kushirikiana na wenzake, mataifa kama Marekani, Canada, Serbia na mabingwa wa dunia Ujerumani nao wako vyema.

KATIE LEDECKY

Ndiye anayeongoza nafasi za medali za Marekani katika mchezo wa kuogelea upande wa wanawake akifanya vyema katika mita 200, 400, 800 na 1,500.

Anapewa nafasi ya kushinda dhahabu ya nne mfululizo ya mita 800, mita 1500, pia kurejesha taji lake la mita 400.

Akiwa na dhahabu saba za Olimpiki na mataji 21 ya Ubingwa wa Dunia, Ledecky tayari ni mmoja wa wababe wa muda wote wa kuogelea na anatarajiwa sana kuongeza idadi yake ya medali Ufaransa.

Nyota mwingine wa kuangaliwa zaidi ni Ariarne Titmus wa Australia, aliyemshangaza Ledecky kuogelea mita 400 mjini Tokyo 2020.

ARMAND DUPLANTIS

Mwamba anashiriki mchezo wa Pole Kuba (pole Vault) na katika Michezo ya Olimpiki ya Tokyo, alifanya makubwa akikimbia mita 6.02 na kushinda medali ya dhahabu katika mbio za wanaume.

Mwanariadha huyo wa Uswizi anayetamba sana ni bingwa wa dunia wa nje mara mbili.

Anashikilia rekodi ya muda wa dunia kwa umbali wa mita 6.24 na huenda akamaliza mita 6.25 msimu huu Paris.

SIMEONE BILES

Raia huyu wa Marekani anachukuliwa ni mmoja wa wachezaji bora wa muda wote wa mchezo wa viungo (Gymnastic) na anatazamiwa kushiriki Olimpiki ya tatu mfululizo.

Alipata nafasi ya kuiwakilisha Marekani baada ya ushindi wake wa raundi zote kwenye majaribio mwezi Juni.

Mshindi huyo mara nne ya medali ya dhahabu ya Olimpiki licha ya kupewa nafasi kubwa ya kushinda, pia ni miongoni mwa nyota wanaotazamwa zaidi katika mashindano hayo kutokana na ubora wake wa kukimbia kisha kuruka kwa mtindo wa aina yake.

Chanzo: Mwanaspoti