Dodoma. Bunge la Bajeti limemalizika. Lakini halikuishia kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya Sh33.1 trilioni na marekebisho ya sheria kadhaa, bali pia miezi takriban mitatu iliyotumika kwa shughuli hiyo ilishuhudia watu sita wakiingia katika msukosuko na Spika Job Ndugai.
Waliokumbana na rungu la Spika Ndugai walidaiwa ama kutoa kauli zilizoonekana kulidhalilisha Bunge, kwenda kinyume na kanuni zake, kuwadhalilisha wabunge na au kutofuata taratibu za chombo hicho cha kutunga sheria.
Katika orodha hiyo, wa kwanza kukumbana na kishindo cha Ndugai katika Bunge hilo lililoanza Aprili 2 hadi Juni 28 kwa wizara 21 kuwasilisha bajeti zake alikuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad baada ya Bunge kutoa azimio la kutofanya naye kazi na kutokana na kutoa kauli yake kuwa Bunge ni dhaifu.
Wengine ni wabunge wawili wa Chadema, Halima Mdee (Kawe) na Godbless Lema (Arusha Mjini) waliosimamishwa kuhudhuria mikutano ya Bunge wakidaiwa kuunga mkono kauli ya Profesa Assad.
Kadhalika, Mbunge wa Shinyanga Mjini (CCM), Stephen Masele naye alikumbana na rungu la Ndugai baada ya kutakiwa kurejea nchini kutoka Afrika Kusini alikokuwa katika vikao vya Bunge la Afrika (PAP) akidaiwa kuzungumza mambo yanayogonganisha mihimili.
Kwa malekezo ya Ndugai, CAG na wabunge hao watatu walihojiwa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kujibu tuhuma zinazowakabili na wote isipokuwa Masele walikutwa na hatia na kuadhibiwa.
Pia Soma
- Rufaa ya Ma DED kutosimamia uchaguzi yaiva, majaji watano kuisikiliza
- Takukuru Dodoma yaeleza ilichobaini ukaguzi robo ya mwaka 2019
- UDSM yabuni mashine ya kisasa ya kutotoreshea vifaranga