Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba amewataka wenyeviti wa Serikali za mitaa mkoani Dar es Salaam kuitisha mikutano kuzungumza na wananchi kuhusu zuio la matumizi ya mifuko ya plastiki nchini litakaloanza Juni Mosi, 2019.
Makamba ametoa kauli hiyo leo Jumanne Machi 21, 2019 katika kikao cha viongozi na watendaji wa Mkoa wa Dar es Salaam wakiwemo wenyeviti wa mitaa yote ya Mkoa huo.
"Mkitoka hapa nendeni mkafanye mikutano na wananchi wa mitaa yenu waelezeni kuhusu zuio hilo wasingoje hadi Juni Mosi. Wananchi wasikie sauti zenu badala ya kusubiri mimi nizungumze katika Televisheni.”
"Kazi ya kusimamisha matumizi ya mifuko ya plastiki imeanza sasa na ikifika Juni Mosi hatupaswi kuwa nayo. Tatizo hawajiandai bado wanatumia na ukiwauliza wanakwambia hadi Juni Mosi," amesema Makamba.
Amesema Serikali haishindwi jambo na kuwataka wenyeviti hao kuwa askari wa Rais John Magufuli katika kufanikisha jambo hilo.
“Siku tulipotangaza kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki tulipata pongezi kutoka katika mataifa mbalimbali. Itakuwa ajabu baada ya siku kadhaa wasikie tumeshindwa jambo hili," amesema Makamba.
Pia Soma
- UVCCM kuwapambania walimu wanaojitolea kupata ajira, posho
- Kenya yataka mjadala wa Jumuiya ya Afrika Mashariki mapambano bidhaa bandia
- Dhamana 11 milioni kwa wizi wa biblia 500
- Dk Tizeba atoa mbinu ya kupata soko la nyama nje ya Tanzania
Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam, Aboubakar Kunenge amesema Mkoa huo umejipanga ipasavyo kuhakikisha utekelezaji wa zuio hilo unafanikiwa.