Dar es Salaam. Rais John Magufuli amesema waliobomolewa nyumba kupisha upanuzi wa barabara ya Morogoro eneo la Kimara hadi Mbezi jijini Dar es Salaam hawatalipwa fidia kwa kuwa walijenga katika eneo la hifadhi ya barabara.
Rais Magufuli ametoa ufafanuzi huo leo Jumatano Desemba 19, 2018 katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi la upanuzi wa barabara hiyo inayofanyika eneo la Kimara Stop Over.
Kiongozi mkuu huyo wa nchi ametoa ufafanuzi baada ya awali mbunge wa Kibamba (Chadema), John Mnyika wakati akiwasalimu waliohudhuria hafla hiyo kumuomba Magufuli kuwalipa fidia wananchi waliokumbwa na bomoabomoa hiyo.
Huku akirejea mara tatu kusema "hakuna fidia", Magufuli amesema hata wakienda mahakamani hakuna fidia.
“Niwambie tu wananchi kuwa ukisogelea barabara madhara yake ni umasikini, hata mimi sijafurahishwa na hii bomoabomoa kwa kuwa wapo ndugu zangu nyumba zao zimebomolewa,” amesema.
"Ni vyema kuwaambia ukweli kesi hii hata wakienda wapi hawawezi kushinda."
Soma Zaidi: Mnyika amwambia Rais Magufuli vyuma vimekaza