Dodoma. Serikali ya Tanzania imesema mkataba wa kampuni ya Rom Solutions co Ltd, Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wa zaidi ya Sh1 trilioni ni moja kati ya mikataba mibovu kuwahi kutokea nchini.
Kauli hiyo imetolewa leo Ijumaa Machi 13, 2020 na Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene mjini Dodoma.
Amesema mkataba huo umevunjwa kwa makubaliano ya pande zote mbili bila kuwepo gharama, kwamba aliyekuwa Kamishina Jenerali wa jeshi hilo, Thobias Andengenye aliingia mkataba huo wenye wa Euro 408,416,238.16 ambazo ni zaidi ya Sh1 trilioni kinyume cha sheria na wala hakuwa na sifa ya kufanya hivyo.
"Kutokana na ukubwa wa mkataba na kiwango cha fedha, kamishina hakuwa na sifa za kusaini kwa kuwa aliyetakiwa kufanya hivyo ni Waziri wa Fedha," amesema Simbachawene.
Amesema Serikali ilivunja mkataba huo Februari 12,2020 bila kuingia hasara ya aina yoyote wala madai ambayo yanadaiwa.
Utata wa mkataba huo uliibuliwa na Rais John Magufuli Januari 23, 2020 na baadaye alitengua uteuzi wa aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola na Andengenye ambao pia waliohojiwa Takukuru pamoja na aliyekuwa katibu mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali Jacob Kingu na naibu katibu mkuu, Ramadhan Kailima.