Dodoma. Mbunge wa Kibakwe (CCM) George Simbachawene amewasilisha azimio la kuitaka Serikali kuharakisha mchakato wa Muswada wa Sheria ya kuifanya Dodoma kuwa makao makuu na kuuleta bungeni.
Akiwasilisha azimio la kumpongeza Rais John Magufuli kwa uamuzi wake wa kuendeleza mji wa Dodoma na kuupa hadhi ya jiji, leo Juni 12 bungeni, Simbachawene amesema ikiwezekana Muswada huo usomwe mara ya kwanza katika mkutano wa 11 unaoendelea.
"Naiomba Serikali kuongeza raslimali fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali itakayoendana na hadhi ya makao makuu na jiji kama vile ujenzi wa Barabara zenye kiwango, miundombinu ya majisafi na majitaka, upimaji na upangaji mzuri wa jiji la Dodoma," amesema.
Simbachawene pia ameliomba Bunge kumpongeza kwa dhati Rais Magufuli na kumuunga mkono kwa uamuzi wake wa kuifanya Dodoma kuwa jiji na hivyo kuliandaa jiji la Dodoma kuendana na hadhi ya Makao Makuu ya Serikali.