WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema serikali inathamini mchango wa wasanii wote waliotunga nyimbo za maombolezo kumuenzi Rais John Magufuli.
Majaliwa alisema hayo jana Zanzibar baada ya kugushwa na wasanii wa muziki wa injili ambao walijitokeza kuimba wimbo wa maombolezo katika shughuli ya kuaga mwili wa Rais Magufuli iliyofanyika kwenye Uwanja wa Amaan.
Mbali na kundi la muziki wa injili kutoka Tanzania Assemblies of God, pia kulikuwa na kundi la muziki wa taarab la The Big Stars ambalo liliimba wimbo wa maombolezo kwa huzuni kuelezea namna walivyohuzunishwa na kifo cha kiongozi huyo aliyefariki dunia Machi 17, mwaka huu.
“Tunashukuru wasanii wote mlioimba nyimbo za maombolezo, tumeona kwaya za dini namna mlivyoshiriki kuomboleza, kazi nzuri endeleeni na tunathamini mchango wenu,” alisema.
Majaliwa alisema nyimbo zote za maombolezo zilizotungwa na wasanii mbalimbali ziendelee kupigwa kwenye vituo vya redio na televisheni kwa siku 21 zilizotangazwa ili kuwafariji Watanzania.
Mwili wa Rais Magufuli jana uliagwa na wananchi wa Zanzibar na leo unatarajiwa kuagwa Mwanza kabla ya kuelekea Chato kwa maziko yatakayofanyika keshokutwa.