Mchekeshaji wa siku nyingi, Amri Athuman maarufu Mzee Majuto jana Ijumaa amewasili kutoka India baada ya kwenda kutibiwa katika Hospitali ya Apollo iliyopo New Delhi, India.
Mzee Majuto alienda India kutibiwa tezi dume baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu, hata hivyo baada ya kuwasili jijini Dar es Salaam amepelekwa katika Hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya kupumzishwa kutokana na uchovu wa safari.
Akizungumza na MCL Digital, Majuto amesema anaendelea vizuri na anamshukuru Mungu pamoja na Rais John Magufuli kwa kuwezesha matibabu yake pamoja na Watanzania kwa ujumla.
Mbali na hayo, Majuto amesema akipona ataachana na kuigiza kwani kwa jinsi alivyoteseka hana hamu ya kuigiza ili apate muda mwingi wa kupumzika.
“Nashukuru afya yangu inaendelea vizuri, namshukuru Rais Magufuli kwa kuwezesha safari yangu na matibabu ya kwenda kutibiwa India.
“Pia nawashukuru Watanzania wote kwa maombi yao, nawapenda sana ila naomba wazidi kuniombea ili nipone haraka na jambo langu la kuwaambia nikipona naacha kuigiza,” anasema Majuto.
Mei 4 mwaka huu alisafirishwa kwenda nchini India kwa ajili ya matibabu baada ya kuugua kwa takribani miezi mitatu.