Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ataongoza ujumbe wa Serikali ya Tanzania katika mazishi ya aliyekuwa mwenyekiti mtendaji wa kampuni za IPP, Reginald Mengi yatakayofanyika kesho Alhamisi Mei 9 kijijini kwake Kisereni Machame wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro.
Taarifa iliyotolewa leo Jumatano Mei 8 na ofisi ya waziri mkuu imeeleza kuwa, ibada ya mazishi ya Mengi itafanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) la Kisereni, Machame ambapo Majaliwa ataongoza ujumbe wa Serikali.
Mwili wa Mengi ambaye alifariki dunia Mei 2 akiwa Dubai, Falme za Kiarabu umeshawasili Moshi mkoani Kilimanjaro leo ukitokea Dar es Salaam na kupokewa na mamia ya wananchi waliojipanga barabarani.
Rais John Magufuli akiwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan na viongozi wengine wa Serikali jana waliongoza maelfu ya wananchi kutoa heshima za mwisho kuaga mwili huo katika ukumbi wa Karimjee, jijini Dar es Salaam.
Hadi mauti yanamfika, Mengi alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Vyombo Vya Habari Tanzania (MOAT). Pia aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).
Baadhi ya nyadhifa ambazo Mengi aliwahi kushika ni pamoja na kamishna wa kamati inayoshughulikia mishahara (SRC), mwenyekiti wa bodi ya wahasibu na wakaguzi Tanzania (NBAA), mwenyekiti wa baraza la taifa la mazingira Tanzania (NEMC); mwenyekiti wa vyombo vya habari Jumuia ya Madola Tanzania, kamishna wa Tacaids na mwenyekiti wa baraza la biashara la Afrika Mashariki.
Habari zinazohusiana na hii
- Mwili wa Mengi wawasili Kilimanjaro, kuzikwa kesho
- VIDEO: Ujenzi wa kaburi la Mengi wafikia hatua za mwisho
- Jinsi Lowassa alivyomzungumzia Mengi