Dodoma. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewatahadharisha Watanzania wanaoishi mabondeni kuhama ili kuepuka athari za mvua zinazoendelea kunyesha nchini.
Majaliwa ameeleza hayo leo Alhamisi Februari 6, 2020 katika kipindi cha maswali ha hapo kwa papo bungeni mjini Dodoma baada ya kuulizwa swali na mbunge wa Viti maalum (CCM), Zainab Vulu.
Zainab amesema mvua zinazonyesha nchini zimesababisha maafa, vifo, watu kupoteza mali zao na uharibifu wa miundombinu na baadhi hawana chakula.
“Je Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia watu hao walioathirika na mafuriko na kuboresha miundombinu nchini kwetu,” amesema Zainab.
Akijibu swali hilo, Majaliwa amesema juzi alikuwa mkoani Lindi katika wilaya ya Kilwa na ameshuhudia maji yamepungua katika maeneo yaliyokumbwa na mafuriko.
Amesema katika maeneo hayo kumetokea uharibifu mkubwa, “nataka niwaambie Watanzania mvua mwaka huu ni nyingi sana. Taasisi yetu ya Hali ya Hewa inaendelea kutuhabarisha kuwa mvua ndio zinaanza na kama inaanza kwa namna hii tutarajie tutakuwa na matukio makubwa ya haya.”
Pia Soma
- Wanaume waaswa kupima saratani ya matiti
- Mvua zaharibu reli, safari kati ya Dar - Dodoma zasitishwa
- Rais TLS ataka sheria, haki kuheshimiwa
“Nitoe wito watu waondoke huku mabondeni iwe kwa shughuli za kilimo na mifugo lakini tusifanye maeneo hayo ya makazi kwa sababu wenzetu wamepoteza nyumba, vyakula na athari nyingine,” amesema.
Amesema kamati za maafa za wilaya na mikoa zimeendelea kufanya kazi na pale kunapokuwa na jambo kubwa watawasiliana na kamati ya maafa ya Taifa ambayo ipo chini ya ofisi yake.