Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameagiza masharti ya utoaji mikopo kwa wajasiriamali kuboreshwa kwa mifuko na 'program' zote za uwezeshaji kufanya tathimini ya kina kuhusiana na huduma zao ili kubaini mafanikio na changamoto katika eneo hilo.
Majaliwa ametoa agizo hilo leo alipokuwa anafungua Maonesho ya Nne ya Mifuko na Programu za Uwezeshaji Wananchi katika Viwanja vya Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha.
“Serikali inataka mikopo itolewe kwa masharti nafuu zaidi na riba ndogo tofauti na sasa ambapo riba ni kubwa na kitu kinachowaumiza wananchi” amesema Majaliwa.
Aidha, Majaliwa ameitaka mifuko inayotoa dhamana kwa wajasiriamali mbalimbali nchini kuimarisha usimamizi, uratibu na utendaji wake kwa kutengeneza mipango maalum ya kila mwaka inayobainisha malengo ya dhamana ziatakazotolewa katika mwaka husika.