WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Hayati Rais Dk John Magufuli ameacha alama ndio maana kila mahali watanzania wanamlilia.
Majaliwa ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Mazishi Kitaifa, ameyasema hayo leo katika uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza akitoa salamu za rambirambi.
“Leo nimekuja na salamu za Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan ameomba tuwe watulivu, tuendelee kufanya shuguli hizi tukiwa na huzuni, anaomba tuendelee kushikamana kushirikiana, kupendana, anayomatumaini katika kipindi hiki si tu tarehe 26 bali siku zote 21 za maombolezo tutaendelea kuwa wamoja.” amesema Majaliwa
Amesema pia Watanzania kila mmoja kwa dini yake waendele kumuombea Rais John Magufuli kwa apumzike kwa amani.
Akitoa utaratibu wa kutoa heshima za mwisho, Makamu wa pili wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar Hemed Suleiman Abdulla ataongoza maombolezo hayo katika Uwanja wa Kirumba , kisha mwili utazungumshwa maeneo mbali mbali ya jiji la Mwanza.
“Tumeona makundi mbali mbali watoto wadogo, wanafunzi, vijana, wazee, wanatamani kumuaga, tumesema jiji la Mwanza liandae barabara maalum ili mwili upite, angalau mpate faraja kuaga.” alisisitiza
Aidha amesema mwili wa Hayati Rais John Magufuli utasimama kwa dakika 10 katika eneo la Busisi ambako ni ukweni kwa marehemu ambapo wazee wa mila na viongozi wa dini watapata nafasi ya kusema machache na kumuombea dua.