Dodoma. Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Godbles Lema amemtaka Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene ajiuzuru.
Lema ametoa kauli hiyo leo Jumapili Februari 2, 2020 katika ukumbi wa Dodoma Hoteli jijini Dodoma, huku akitaja sababu ni watu waliokufa wakati wakikanyaga mafuta Mjini Moshi.
Mbunge huyo wa Arusha mjini, ametoa kauli hiyo ikiwa ni saa chache tangu Waziri wa Simbachawene alipotoa kauli ya pole na taarifa za kukamatwa kwa Nabii na Mtume Boniface Mwamposa.
Amesema hali ilivyokuwa Moshi, ilipaswa IGP, RPC, OCD na Waziri waachie ngazi kwa sababu ya uzembe uliofanyika.
“Haiwezekani umati kama ule ukakosa ulinzi wa polisi au zimamoto, Waziri hatoshi huyu ameanza vibaya, namshauri ajiuzuru ili arudi mtaa tena akafikiriwe upya,” amesema Lema.
Kwa mujibu wa Lema, kitendo cha kutuhumu kanisa au Mchungaji ni uonevu kwa kuwa wao hawana uwezo wa kuzuia imani ya watu na hasa inapofika wakati kama ule.
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Nabii Mwamposa adaiwa kukaidi kibali alichopewa na Polisi
- Nabii Mwamposa aaga waumini Dar aelekea Moshi kuitikia wito wa Polisi
- VIDEO: Majeruhi asimulia tukio zima la Mchungaji Mwamposa kumwaga mafuta ya upako
- VIDEO: Polisi Tanzania wamtaka Mtume Mwamposa kujisalimisha