RAIS Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete amefafanua kuwa Machi 2, 2020 alitegemea kukabidhiwa nyumba na Hayati Rais Dk John Pombe Magufuli iliyojengwa na Serikali, lakini ilishindikana kutokana na changamoto mbalimbali.
Akizungumza wakati wa kutoa salamu za maombolezo, Kikwete alisema lengo lilikuwa kwa pamoja na Hayati Rais John Magufuli kuishi kwenye nyumba hiyo baada ya kustaafu.
“Alitakiwa kunikabidhi nyumba aliyonijengea bahati mbaya haikuwezekana, natamani turudishe siku nyuma kidogo angalau tupate picha ya mwisho ya ukumbusho, tungetaniana, Mwenyezi Mungu amepitisha hukumu yake, haijatokea na haitatokea.” alisema Kikwete.
Alisema usiku wa Machi 17 hatousahau katika maisha yake baada ya kupata taarifa za kifo cha hayati Magufuli kupitia jumbe fupi alipokuwa akizungumza na ndugu zake kijiji kwao Msoga, hivyo ilimlazimu kuahirisha mazungumzo na kutafuta ukweli wa taarifa hiyo.
“Niliwaaga ndugu zangu kuwambia warudi makwao bila kuwambia nini kimetokea nikakatiza mazungumzo yao, nikaingia ndani nikasema hii ni kweli au uzushi, nililia, moyo uliuma sana, sikulia kwa sauti lakini machozi yalinitoka,”alisema Kikwete.
Alisema kuwa alipewa kiwanja na hayati Magufuli kilichopo Chato na kumtaka ajenge nyumba ili wawe majirani katika kuimarisha uhusiano na urafiki wao wa muda mrefu.
“JPM alinikabidhi kiwanja Chato, akanikabidhi na hati, akaniambia we Mkwere haya ujenge, nikamwambia nisipojenga akaniambia utajua. Ilikuwa nimatamanio yangu akimaliza urais wake siku moja tuwe majirani tukae pamoja.”alisema Kikwete