Dar es Salaam. Oktoba 11, 2018 saa 11:30 alfajiri mfanyabiashara maarufu nchini, Mohammed Dewji alitekwa wakati akiwa katika Hoteli ya Colosseum Oysterbay jijini Dar es Salaam.
Tangu siku hiyo hadi leo mchana Jumanne Oktoba 16, 2018 hakuna taarifa zozote za watekaji, lengo la kumteka wala fununu za alikohifadhiwa Mo Dewji ambaye miaka mitatu iliyopita jarida la Forbes lilimtaja kuwa tajiri namba moja Afrika kwa vijana walio chini ya miaka 40.
MCL Digital imekuchambulia mambo yaliyotokea na kuzungumzwa kuhusu tukio hilo tangu lilipotokea hadi leo.
Viongozi wamiminika hotelini
Takribani saa mbili tangu Mo Dewji kutekwa askari polisi na viongozi mbalimbali walifika katika hoteli ya Colosseum.
Baadhi ya waliojitokeza ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa pamoja na maofisa kadhaa wa usalama.
Ulinzi ulikuwa mkali katika eneo hilo wakati maofisa wa polisi wakifanya uchunguzi wa awali kwa kutumia vipimo mbalimbali.
Mambosasa ataja wahusika wa utekaji
Muda mchache baada ya kufika katika eneo la tukio, Mambosasa aliwaeleza waandishi wa habari kuwa Mo Dewji alitekwa na Wazungu wawili waliokuwa katika gari aina ya Toyota Surf, kwamba kulikuw ana magari mawili, moja lilikuwa ndani na jingine nje ya hoteli hiyo. Alisema wahusika walikuwa wamefunika nyuso zao.
VIDEO: Mambosasa asema waliomteka Mo Dewji ni Wazungu
VIDEO: Polisi Tanzania waeleza mwanzo mwisho utekaji wa bilionea Mo Dewji
Uvumi wazagaa Dewji amepatikana
Kuanzia saa sita mchana Oktoba 11, 2018 taarifa za kupatikana kwa mfanyabiashara huyo zilianza kuzagaa ikidaiwa kuwa zimetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.
Makonda akanusha
Taarifa hizo zilikanushwa na Makonda na kubainisha kuwa huenda waliotoa taarifa hizo walimnukuu vibaya.
Makonda akanusha Dewji kupatikana, watu wamiminika nyumbani
Manara akamatwa na polisi
Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara alikamatwa na polisi kutokana na tukio la kutekwa kwa Mo Dewji kutokana na kusambaza taarifa za tukio hilo kwenye mitandao ya kijamii kwa madai ya kutumwa na familia, jambo ambalo lilidaiwa kuwa si kweli.
Manara alikamatwa Oktoba 11 jioni na kuachiwa kabla ya kukamatwa tena Oktoba 12, 2018 asubuhi.
Manara akamatwa Dar, ahojiwa tukio la kutekwa Mo Dewji
Lugola azungumza
Jumamosi, Oktoba 13, 2018 Waziri wa Mambo ya Ndani Kangi Lugola alizungumza na vyombo vya habari na kubainisha kuwa polisi inaendelea na mchakato wa kumtafuta mfanyabiashara huyu.
Aliwaeleza wanahabari kuwa wakati huo watu 20 walikuwa wakishikiliwa na polisi akataka ndani ya saa 24 watu wanaowashikilia kwa uchunguzi kuhusiana na tukio hilo mara baada ya kuwahoji na kubaini hawahusiki au hawana taarifa kamili waachiliwe.
Live Lugola akizungumzia matukio ya utekaji
Wanaoshikiliwa na polisi wafikia 26
Hadi kufikia Jumapili, Oktoba 14 idadi ya watu waliokuwa wakishikiliwa kwa mahojiano kuhusu tukio la kutekwa kwa Dewji ilifikia 26, Manara.
Jeshi la polisi lilisema hatua hiyo ni sehemu ya kazi ya uchunguzi na baada ya kukamilisha kuwahoji taarifa zaidi ingetolewa.
Masauni na CCTV
Jumapili Oktoba 14, 2018 Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Masauni alisema Serikali inatarajia kusambaza kamera maalum za CCTV katika miji mikubwa na baadhi ya mikoa ili kukabiliana na matukio ya uhalifu.
Kutekwa kwa Mo Dewji, Serikali yasema itafunga CCTV miji mikubwa
Sh1 bilioni kutolewa
Jumatatu mchana, Oktoba 15, 2018 familia ya Dewji ilitangaza donge nono la Sh1 bilioni kwa yoyote atakayefanikisha kupatikana kwa mfanyabiashara huyo na kwamba familia hiyo imeahidi kumlinda mtoa taarifa hizo.
Familia ilitangaza namba za simu zitakazotumika kukusanya taarifa zitakazosaidia kupatikana kwa bilionea huyo.
KUTEKWA KWA MFANYABIASHARA MO DEWJI: Familia yatangaza dau la bilioni moja
19 waachiwa kwa dhamana
Leo Oktoba 16, 2018 Mambosasa alisema watu 19 kati ya 26 waliokuwa wakishikiliwa na polisi wakihusishwa na tukio la kutekwa mfanyabiashara huyo wameachiwa kwa dhamana, akiwemo Manara.
Soma zaidi:
19 akiwemo Haji Manara waachiwa kwa dhamana tukio la kutekwa Mo Dewji