MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam imesema sababu zilizotolewa na mdhamini wa aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kuwa mshitakiwa huyo yupo mikoani kutafuta wadhamini, hazikubaliki kisheria.
Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba alisema jana kuwa suala la mshitakiwa kugombea ubunge au udiwani haliihusu Mahakama na imemtaka mdhamini huyo, Robert Katula ahakikishe anampeleka mshitakiwa mahakamani Septemba 14 mwaka huu.
Hakimu Simba aliyasema hayo wakati kesi ya uchochezi inayomkabili, Lissu na wenzake ilipotajwa. Mbali na Lissu mshitakiwa mwengine ambaye hakufika mahakamani ni Ismail Mehboob.
Mdhamini wake, Juma Othman alidai kuwa mshitakiwa anaumwa na alitoa nyaraka kudhibitisha kuwa mshitakiwa ni mgonjwa. Mdhamini wa Lissu, Katula alidai kuwa jana asubuhi aliwasiliana na mshitakiwa huyo akamweleza kuwa yuko mkoani anatafuta wadhamini kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu.
Aliahirisha kesi hiyo hadi Septemba 14 mwaka huu kwa kutajwa. Washitakiwa wengine kwenye kesi hiyo ni Simon Mkina, Mhariri wa gazeti la Mawio, Jabir Idrisa na Mchapishaji wa Kampuni ya Jamana, Ismail Mehboob