Wakati Serikali, wadau na jamii kwa ujumla ikipambana kukabiliana na ukatili dhidi ya watoto, matukio ya ubakaji na ulawiti yameendelea kuripotiwa katika maeneo kadhaa nchini.
Mkoani Kilimanjaro inaripotiwa kuwa, katika Kijiji cha Kifuni, Kata ya Kibosho Magharibi, wilayani Moshi, Wenseslaus Olomi (50), amejiua kwa kujinyonga ikidaiwa ni baada ya kufumaniwa akimbaka mjukuu wake wa miaka sita.
Olomi inadaiwa kabla ya kujiua, mke wake alimfumania akimbaka mjukuu wake, hivyo alipiga yowe kuomba msaada ndipo alipomtaka mama huyo aondoke nyumbani na asipofanya hivyo atachukua uamuzi wa kumuua.
Inaelezwa baada ya mke wake kupata vitisho hivyo, aliondoka nyumbani na kwenda kutafuta sehemu nyingine ya kuishi.
Aliporejea Septemba 2, alikuta mlango upo wazi huku mwili wa mume wake ukining’inia juu ya kenchi ya nyumba akiwa amejinyonga kwa kutumia shuka.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa amethibitisha tukio hilo. Amesema chanzo cha tukio hilo ni mgogoro wa kifamilia.